20.4 C
New York

Visual| Daraja la Busisi kutoka dakika 120 hadi 4

Published:

Na Immaculate Makilika – MAELEZO

Kawaida daraja hujengwa kwa kusudi la kuwa na njia ya kupitia juu ya pengo au kizuizi. Licha ya hivyo daraja pia linaweza kuchochea uchumi wa eneo husika kwa kuwa na faida lukuki ikiwemo usafiri na usafirishaji wa watu na bidhaa.

Akizungumza Juni 14, 2023 jijini Mwanza wakati wa kukagua maendeleo ya mradi wa ujenzi wa daraja la Kigongo – Busisi linalotajwa kuunganisha barabara kuu ya Usagara – Sengerema, Geita katika Ziwa Victoria,  sambamba na kuunganisha  watu wa mikoa ya Mwanza, Geita, Kagera na nchi jirani ya Uganda, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzanzia, Dk. Samia Suluhu Hassan aliwashukuru wananchi wa Mwanza na maeneo ya karibu kwa kutoa ushirikiano tangu kuanza kwa ujenzi wa daraja hilo hadi hatua ilipofikia.

“Daraja hili litakapokamilika ni faida  kwa Watanzania wote lakini na kwenu nyie mlio karibu nalo, daraja hili limeanza kutoa ajira kwenu na litaendelea kutoa ajira kwa kuwa magari yatapita hapa kwenda maeneo mbalimbali, lakini niwaombe na wale wenye tabia ya wizi wa vifaa vya ujenzi waache na niwapongeze kwa kutoa ushirikiano wakati wote wa ujenzi”, alisema Rais Samia.

Kwa upande wake, Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS), Mhandisi Mohamed Besta alisema kuwa kutokana na idadi kubwa ya magari yanayovuka kwa siku  kivuko hutumia takribani hadi saa 2 kutoka upande mmoja kwenda mwingine, baada ya daraja kukamilika muda wa kuvuka Ziwa Viktoria unatarajiwa kupungua hadi kuwa takribani dakika nne.

Akifafanua baadhi ya manufaa ya daraja hilo linalotajwa kuwa daraja refu kuliko yote Afrika Mashariki na Kati na la sita katika bara la Afrika mara baada ya kukamilika kwake.

Mhandisi Besta alisema: “Baada ya daraja kukamilika itarahisisha usafiri wa majira yote ya mwaka kwa saa 24 na kumaliza tatizo la msongamano wa magari unaotokea kila mara na kuwa kichocheo cha uchumi katika ukanda wa Ziwa Viktoria na taifa kwa ujumla kwani mazao ya wakulima na mazo ya samaki yataweza kufika sokoni kwa wakati,”.

Aidha, Mhandishi Besta aliendelea kwa kusema kuwa ujenzi wa daraja hilo la Kigongo – Busisi ambalo ni kilomita tatu na barabara unganishi ni km 1. 66 linalofadhiliwa na Serikali kwa asilimia 100 unagharimu Sh bilioni 716.33,  ujenzi wake ulianza Februari 25, 2020 na unatarajiwa kukamilika Februari 24, 2024.

Aidha, kwa ujumla hatua ya utekelezaji wa mradi huo  hadi sasa ni asilimia 75, na tayari  mkandarasi ameshalipwa Sh bilioni 368.67, Mhandisi mshauri amelipwa Sh bilioni 4, aidha, Sh billioni 3 zimetumika kufidia wananchi.

Mradi huo umetoa ajira zaidi ya 700 huku Watanzania wakipata sehemu kubwa ya ajira hizo, ambapo wafanyakazi 56 pekee ndiyo wageni kutoka nje ya nchi.

Kwa upande wao baadhi ya wafanyakazi wanaofanya kazi katika mradi huo waliipongeza serikali kwa kutoa wazo hilo kuwa mbali na kutengeneza ajira, litarahisisha usafirishaji wa bidhaa na huduma za watu pamoja na kuchochea uchumi.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan akizungumza na Wananchi wa Kigongo Ferry Wilayani Misungwi mara baada ya kukagua Daraja la JP Magufuli mkoani Mwanza Juni 14, 2023.

Hili itakuwa katika madaraja matatu bora barani Afrika. Daraja hilo litakalokuwa na uwezo wa kubeba hadi tani 180 lina uwezo wa kuchukua hadi magari 1,600 kwa wakati mmoja, hatua ambayo itakuwa na mchango mkubwa katika kuharakisha maendeleo mkoani Mwanza kwa kuwa kitovu cha biashara katika Ziwa hilo.

Ikumbukwe kuwa utekelezaji wa mradi huo ni sehemu ya utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM inayoashiria kuwa Chama kitaisimamia Serikali katika kukamilisha madaraja saba ambayo ni Salender na Gerezani (Dar es Salaam), Wami (Pwani), Kigongo- Busisi (Mwanza), Kitengule (Kagera), Msingi (Singida) na Malagarasi kando ya barabara ya Kabingo-Kasulu-Manyovu mjini Kigoma.

Related articles

spot_img

Recent articles

spot_img