WASHINGTON DC, Marekani
RAIS wa zamani wa Honduras, Juan Orlando Hernandez, ametoka gerezani kwa msamaha wa Rais wa Marekani, Donald Trump. Orlando Hernandez alikuwa akitumikia kifungo cha miaka 45 gerezani nchini Marekani kwa kosa la kuingiza dawa za kulevya aina ya cocaine na kumiliki silaha kinyume cha sheria.
Alikutwa na hatia Machi, mwaka jana na alikuwa akitumikia kifungo chake katika Gereza la USP Hazelton mjini Virginia. Hivi karibuni, Rais Trump alitumia mitandao ya kijamii kuzungumzia maisha ya Hernandez huko gerezani, akisema mwanasiasa huyo amekuwa akifanyiwa ukatili.
Kwa upande wake, mke wa Hernandez, Ana García de Hernandez, ametumia mitandao ya kijamii kumshukuru Rais Trump kwa msamaha huo kwa mumewe.
Hernandez aliyekuwa Rais wa Honduras kuanzia mwaka 2014 hadi 2022 alikamatwa na kupelekwa Marekani kwa ajili ya kusomewa mashitaka ya kuingiza dawa za kulevya nchini humo. Mbali ya kuhukumiwa kifungo cha miaka 45, pia adhabu hiyo ilienda sambamba na faini ya Dola za Marekani milioni 8.


