33.3 C
New York

Hii ndiyo Siku ya Nelson Mandela

Published:

Na mwandishi wetu, Gazetini

JULAI 18 ya kila mwaka ni Siku ya Kimataifa ya kumbukizi ya mchango mkubwa alioutoa Nelson Mandela katika ulimwengu wa siasa, hasa kwa mapambano na ushindi wake dhidi ya ubaguzi wa rangi nchini kwake, Afrika Kusini.

Umoja wa Mataifa (UN) uliitangaza Julai 18 kuwa maalumu kwa Mandela, ikizingatiwa kuwa pia ndiyo siku ya kusherehekea kumbukizi ya kuzaliwa kwake (birthday).

UN ilianza kuitambua Siku hiyo Novemba, 2009, na maadhimisho ya kwanza ya Umoja huo kumuenzi Mandela yalifanyika Julai 18, 2010.

Mwaka 2014, Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa liliasisi Tuzo ya Nelson Mandela, ambayo hutolewa kila baada ya miaka mitano kutambua mchango wa watu waliojitoa kutetea haki za binadamu.

Moja ya alama zisizofutika katika historia ya Mandela ni kusota gerezani miaka 27 akipigania haki za watu weusi nchini Afrika Kusini.

Ni baada ya mateso hayo, aliingia madarakani kuiongoza nchi hiyo mwaka 1994, akiandika historia ya kuwa Rais wa kwanza mweusi na aliyechaguliwa kidemokrasia.

Hata hivyo, kuelekea Julai 18, safari hii Siku ya Mandela inaadhimishwa wakati Afrika Kusini ikiwa imegubikwa machafuko ya aina nyingine ya ubaguzi.

Tofauti na ubaguzi wa rangi alioupinga na kuuondosha Mandela, kwa sasa wananchi wa Afrika Kusini wamemezwa na chuki dhidi ya raia wa kigeni wanaoishi nchini humo.

Maelfu ya raia wa Nigeria, Malawi, Msumbiji na Ghana wamelazimika kukimbia na kurejea makwao wakihofia kuuawa katika vurugu hizo za wazawa.

Related articles

Recent articles