Na Mwandishi Wetu,Gazetini
Mbunge wa Jimbo la Tunduru Kaskazini wa Chama cha ACT Wazalendo, Ado Shaibu, amesema watanzania wanalitazama kwa umakini mkubwa Bunge la 13 ili kubaini kama litakuwa Bunge lenye matumaini kwa Wananchi.
Shaibu ametoa kauli hiyo leo, Jumanne Novemba 11, 2025, Bungeni jijini Dodoma, mara baada ya Bunge kumchagua Mbunge wa Jimbo la Ilala (CCM), Mussa Azzan Zungu, kuwa Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, baada ya kupata kura 378 kati ya kura 383 zilizopigwa.
Akizungumza baada ya uchaguzi huo, Mbunge Shaibu amesema matarajio yake ni kuona Bunge hilo likitekeleza wajibu wake ipasavyo kwa mujibu wa Katiba na Sheria za nchi.
“Matarajio yangu ni kwamba Bunge litafanya kazi yake ya kikatiba na kisheria. Bunge ni chombo cha kuisimamia Serikali, siyo chombo cha kuisifia hata pale inapokosa kustahili, ni jukumu letu kuhakikisha tunasimamia masilahi ya Wananchi na kutunga Sheria zenye manufaa kwa Taifa,” amesema Shaibu.


