Na Mwandishi Wetu
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Samia Suluhu Hassan ametunukiwa Medali ya ‘Mother of the Nation Order’ kutoka kwa Rais wa Umoja wa Falme za Kiarabu(UAE) , Sheikh Mohamed bin Zayed Al Nahyan.
Medali hiyo iliwasilishwa na Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Mambo ya Nje wa Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE), Sheikh Abdullah Bin Zayed Al Nahyan Ikulu Jijini Dar es Salaam Mei 05,2025.
Medali hiyo ni moja kati ya medali za juu kutoka kwa UAE. Hutolewa kwa kutambua mchango kiongozi katika kuleta maendeleo endelevu kwa jamii yake.
Serikali ya UAE imetambua mchango mkubwa wa Rais Samia katika kuwaletea Watanzania maendeleo endelevu ambayo yanaendana na Sera za UAE za maendeleo endelevu katika kijamii, uwezeshaji wanawake na ushirikiano wa kimataifa.
Sheikh Abdullah aliwasilisha salamu kutoka kwa Rais wa Umoja wa Falme za Kiarabu, kuwatakia kheri wananchi wa Tanzania katika maendeleo pamoja na ustawi zaidi. Pia alisisitiza kuimarishwa zaidi uhusiano wa kudumu baina ya nchi hizo mbili na kupanua ushirikiano katika sekta muhimu.