19.4 C
New York

Morocco, Brazil zatinga hatua ya 32 bora, Qatar yaaga

Published:

SEATTLE, Marekani

MOROCCO imefuzu hatua ya 32 bora ya Kombe la Dunia 2026 baada ya kuibuka na ushindi wa mabao 4-2 dhidi ya Haiti katika mchezo wa Kundi C uliochezwa mapema Alhamisi.

Katika mechi hiyo, Achraf Hakimi na Ismail Saïbari waliifungia Morocco mabao ya kipindi cha kwanza kabla ya Soufiane Rahimi na Yassine Jassim kuongeza mengine mawili kipindi cha pili na kuhitimisha ushindi huo muhimu.

Ushindi huo umeihakikishia Morocco tiketi ya kusonga mbele kutoka Kundi C, sambamba na Brazil ambao pia wamefuzu baada ya kuichapa Scotland mabao 3-0 na kumaliza vinara wa kundi hilo.

Morocco na Brazil zilikuwa tayari katika nafasi nzuri ya kusonga mbele kabla ya michezo ya raundi ya tatu, baada ya kila moja kuwa imejikusanyia pointi nne katika mechi mbili za mwanzo. Hivyo, michezo yao ya mwisho ilibeba zaidi ushindani wa kuwania kufuzu pamoja na kumaliza kileleni mwa kundi.

Wakati Morocco na Brazil zikisherehekea kutinga hatua inayofuata, hali ilikuwa tofauti kwa Qatar, ambao wameaga rasmi mashindano hayo baada ya kufungwa mabao 3-1 na Bosnia na Herzegovina katika mchezo uliochezwa Seattle, Marekani.

Katika mechi nyingine ya Kundi B, Uswisi iliibuka na ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Canada, moja ya nchi wenyeji wa mashindano hayo, katika mchezo uliofanyika Vancouver. Ushindi huo umeifanya Uswisi kufuzu ikiwa kinara wa kundi, huku Canada nayo ikitinga hatua ya 32 bora baada ya kumaliza ya pili.

Kwa matokeo hayo, Qatar imehitimisha kampeni yake ya pili katika historia ya Kombe la Dunia, baada ya ushiriki wake wa kwanza kuwa mwaka 2022 ilipokuwa mwenyeji wa mashindano hayo. Qatar imeondoka ikiwa na pointi moja pekee.

Uswisi imemaliza kileleni mwa Kundi B kwa pointi saba, ikifuatiwa na Canada yenye pointi nne. Bosnia na Herzegovina nayo imefikisha pointi nne, lakini imebakia nafasi ya tatu kwa tofauti ya mabao dhidi ya Canada, huku matumaini yake ya kusonga mbele yakibaki katika nafasi ya kuingia hatua ya 32 bora kama moja ya timu nane bora zilizomaliza katika nafasi ya tatu.

Related articles

Recent articles