NEW JERSEY, Marekani
TIMU ya soka ya Taifa ya Senegal iliingia kwenye fainali za Kombe la Dunia za mwaka huu (2026) ikiwa inapewa nafasi kubwa ya kufanya vizuri.
Hata hivyo, mambo yamekuwa tofauti na sasa timu hiyo haijaambulia hata sare, achilia mbali ushindi, katika mechi mbili ilizocheza.
Kama watashindwa kuifunga Iraq katika mchezo wa mwisho utakaochezwa Ijumaa ya wiki hii, safari yao kwenye michuano ya msimu huu itakuwa imeishia hapo.
Hata hivyo, kile kinachotajwa kuwa sababu ya mwenendo mbaya wa timu hiyo ni mazingira mabovu ya kambi yao mjini New Jersey, Marekani.
Wachezaji na viongozi wao wanaishi kwenye hoteli ya nyota nne iitwayo Hyatt Regency, tofauti na matatajio ya hoteli ya nyota tano kama zilivyo timu zingine kubwa kwenye mashindano hayo.
Ni hoteli ya kiwango cha chini kuliko Fairmont Palace waliyoweka kambi wakati wa fainali za AFCON 2025 nchini Morocco.
Mbali na daraja la hoteli, pia zimekuwapo taarifa mbaya juu ya ubora wa vyakula. Ni vyakula vya ‘kawaida’ tofauti na matatajio ya wengi ndani ya kambi.
Senegal imesafiri na mpishi lakini si yule aliyekuwapo katika michuano mingi iliyopita. Aliondoka baada ya mechi ya kirafiki dhidi ya Saudi Arabia ya kujiandaa na Kombe la Dunia.
Mpishi wa sasa, kwa mujibu wa wafanyakazi waliopo kwenye msafara wa timu hiyo Kombe la Dunia, hajafikia viwango vya upishi alivyokuwa navyo mtangulizi wake, ambaye aliacha kazi kwa sababu binafsi.
Hiyo imesababisha utulivu mdogo kwenye timu kwani imekuwapo ingia, toka ya kwenda kutafuta vyakula nje ya kambi.
Ajabu nyingine ni hii ya taarifa zinazodai kuwa baadhi ya viongozi wa Shirikisho la Soka (FSF) wamewasafirisha ndugu zao na wanaishi jirai kabisa na hoteli waliyopo wachezaji.
Pia, familia za wachezaji ziko jirani na hoteli hiyo, huku gharama zote zikilipwa na uongozi wa FSF.
Kama hiyo haitoshi, ni hivi karibuni tu wachezaji na wafanyakazi walilipwa posho walizokuwa wanadai kwa muda mrefu.
Isisahaulike pia, kocha mkuu, Thiaw, amesafiri na timu akiwa hana mkataba mpya. “Hata kama nitatwaa ubingwa wa Kombe la Dunia, nitajiuzulu baada ya fainali hizi,” amesema.
Senegal inaisubiri Iraq baada ya kupoteza mechi mbili za awali dhidi ya Ufaransa (3-1) na Norway (3-1).


