Na mwandishi wetu, Gazetini
LEO ni Januari Mosi, 2026, tukiwa na miezi 12 ya kuhesabu ili kuumaliza mwaka huu. Mwaka 2025 umekwenda zake. Hata hivyo, kwa wapenzi wa soka, 2025 ulikuwa ni mwaka ulioshuhudia matukio makubwa mengi. Makala haya yaangazia hilo.
Chelsea mabingwa wa dunia
Wakati wa majira ya kiangazi, kulikuwa na michuano ya fainali za Kombe la Dunia kwa ngazi ya Klabu. Ni mashindano ya Shirikisho la Soka la Kimataifa (FIFA).
Ikishirikisha timu 32 zilizokutana Marekani, michuano hiyo ilimalizika kwa Chelsea kutwaa ubingwa ikiifunga PSG mabao 3-0 katika mchezo wa fainali.
Ikumbukwe, hilo lilikuwa taji la pili ndani ya mwezi mmoja kwa Blues baada ya kuwa mabingwa wa Ligi ya Europa Conference.
‘Lionesses’ tishio kwa wanawake
Timu ya taifa ya England kwa upande wa soka la wanawake ilitetea taji lao la fainali za Mataifa ya Ulaya (EURO). Lionesses walianza vibaya kwa kufungwa na Ufaransa, kabla ya kuitoa Sweden kwa penalti katika mchezo wa hatua ya 16 Bora ya michuano hiyo iliyofanyika Uswis.
Katika mchezo wa fainali, walikutana na Hispania, ambapo Lionesses walitwaa ubingwa kwa ushindi wa mikwaju ya penalti, shujaa akiwa ni kipa wao, Hannah Hampton.
PSG watimiza ndoto yao
Licha ya ubabe wao katika soka la Ufafansa, ndoto ya muda mrefu kwa PSG ilikuwa ni ubingwa wa michuano ya Ligi ya Mabingwa Ulaya. Walitimiza ndoto hiyo mwaka 2025 kwa kuifunga Inter Milan mabao 5-0 katika mchezo wa fainali uliochezwa jijini Munich, Ufaransa.
Kane naye atwaa ubingwa
Akiwa na Tottenham, Harry Kane aliweka na kuvunja rekodi nyingi Ligi Kuu ya England lakini hakuwahi kutwaa ubingwa wa michuano mikubwa. Mwaka 2025 ulikuwa wa kutimiza ndoto hiyo.
Aliiongoza Bayern Munich kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu ya Ujerumani (Bundesliga). Ni msimu ambao Kane, nahodha wa timu ya taifa ya England, alifunga mabao 41 katika michuano mbalimbali.
Conte tishio Serie A
Antonio Conte aliiongoza Napoli kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu ya Italia (Serie A). Taji la pili la Ligi kwa timu hiyo ndani ya misimu mitatu.
Ni msimu ambao Napoli ikimtegemea zaidi Romelu Lukaku aliyefunga mabao 14, pia kiungo Scott McTominay akiwa kwenye kiwango bora.
Conte, kwa upande wake, lilikuwa ni taji la sita la Ligi Kuu baada ya kubeba akiwa na Juventus, Chelsea na Inter Milan.
Southgate aaga England
Baada ya miaka mingi ya kuliongoza benchi la ufundi tangu alipopandishwa akitokea timu ya vijana, Southgate alijiuzulu kuinoa timu ya taifa ya England.
Nafasi yake amechukua kocha wa zamani wa Chelsea, Thomas Tuchel, ambaye mtihani aliopewa ni kuipa England ubingwa wa Kombe la Dunia katika fainali za mwaka huu.


