Na Mwandishi Wetu, Gazetini
Juni 8, 2025, Tanzania iliungana na mataifa mengine duniani kuadhimisha Siku ya Bahari Duniani — siku muhimu ya kutoa wito wa kimataifa wa kulinda bahari, chanzo kikuu cha maisha na uhai wa sayari.
Bahari zenye afya ni msingi wa bioanuwai, ustawi wa kiuchumi, usalama wa chakula na kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi. Kwa kutambua umuhimu huo, Serikali ya Tanzania ilizindua mwaka jana Sera ya Taifa ya Uchumi wa Buluu ya 2024 inayolenga kutumia fursa za bahari kwa njia endelevu na jumuishi.
Uchumi wa buluu unajumuisha sekta kama uvuvi, ufugaji samaki, nishati ya baharini, usafirishaji, utalii wa fukwe, utafutaji wa madini na teknolojia ya baharini. Kwa mujibu wa OECD, thamani ya uchumi wa bahari duniani ilikuwa Dola trilioni 1.5 mwaka 2010 na inatarajiwa kuongezeka mara mbili ifikapo 2030 endapo mazingira ya bahari yatatunzwa.
Hata hivyo, bahari zinakabiliwa na changamoto kubwa zikiwemo uvuvi wa kupindukia na uchafuzi wa mazingira. Takriban asilimia 80 ya uchafu wa bahari hutoka nchi kavu, ukiwemo plastiki, mbolea na maji taka, hali inayoharibu viumbe wa baharini na kutishia maisha ya jamii.
Ripoti ya FAO ya The State of World Fisheries and Aquaculture 2024 inaonesha kushuka kwa samaki walioko katika viwango salama vya uvuvi kutoka asilimia 90 mwaka 1974 hadi asilimia 62 mwaka 2021, huku uvuvi wa kupindukia ukifikia asilimia 38.

Kupitia Sera ya Uchumi wa Buluu, Tanzania imeanza kuchukua hatua. Mfano ni Seaweed Café, biashara ya kijamii inayotumia mwani kama bidhaa ya chakula na lishe. Nancy Iraba, Mkurugenzi Mtendaji wa Seaweed Café anasema: “Kwa Seaweed Café, mwani si tu zao la biashara bali suluhisho la afya, mazingira na uchumi… hasa kwa wanawake wakulima.”
Naye Peter Knights wa shirika la Wild Africa ameongeza:“Bahari zetu zinabeba maisha ya dunia. Ni wajibu wetu kuzilinda dhidi ya uchafuzi na uvuvi usioendelevu.”
Wananchi wanahimizwa: Kukataa bidhaa za uvuvi usioendelevu, kupunguza matumizi ya plastiki, kusaidia usimamizi wa uvuvi unaotegemea sayansi na jamii na kusema kwa sauti juu ya sera bora za kulinda bahari.
Kwa ushirikiano kati ya Serikali na wananchi, Tanzania inaweza kuwa mfano bora wa mafanikio ya Uchumi wa Buluu unaolinda mazingira na kuboresha maisha ya watu.


