CAIRO, Misri
KOCHA wa Al Ahly, Jess Thorup, amekosoa kitendo cha kukosekana kwa teknolojia ya kumsaidia mwamuzi kwa marudio ya video (VAR) katika mechi za hatua ya makundi ya Ligi ya Mabingwa Afrika.
Thorup raia wa Denmark ameyasema hayo kuelekea mchezo wao wa leo ugenini dhidi ya FAR Rabat ya Morocco.
Al Ahly watacheza mechi yao ya pili ya Kundi B baada ya ushindi wa mabao 4-1 dhidi ya JS Kabylie ya Algeria.
“Ni muhimu sana kwa sababu inatoa haki, hasa katika matukio tata. Sijui sababu ya kukosekana kwake lakini tuheshimu mfumo wa waamuzi, ingawa pia teknolojia imekuwa na umuhimu mkubwa katika mechi za aina hii,” alisema.
Wakati huo huo, kocha huyo mwenye umri wa miaka 55 alizungumzia kiwango kizuri kilichooneshwa na timu yake katika mchezo dhidi ya JS Kabylie.
“Tumeanza vizuri kwa ushindi wa raundi ya kwanza dhidi ya JS Kabylie. Kiwango kilikuwa kizuri na tunapambana kukiendeleza na kupata matokeo mazuri …”
Mechi nyingine ya Kundi B kwa siku ya leo ni ile itakayozikutanisha Yanga na JS Kabylie huko Algeria.
Published:


