24 C
New York

Sura 8 tofauti vita ya Yanga, Wabotswana

Published:

Na mwandishi wetu, Gazetini

YANGA watashuka dimbani katika ardhi ya ugenini mjini Gaborone, Botswana, kesho Septemba 5, 2026, kwa mchezo wa hatua ya awali ya msimu huu wa Ligi ya Mabingwa Afrika.

Mechi yao dhidi ya Gaborone United inatarajiwa kuchezwa katika Uwanja wa Taifa wa Botswana, huku Yanga wakihitaji ushindi au walau sare ili kujiweka katika mazingira mazuri kuelekea mchezo wa marudiano wiki moja baadaye jijini Dar es Salaam.

Wawakilishi hao wa Tanzania watashuka dimbani wakiwa na mwenendo mzuri tangu msimu huu uanze, ambapo wameshinda mechi zote tano za Ligi Kuu, achilia mbali ile ya Ngao ya Jamii waliyoifunga Simba bao 1-0.

Je, Gaborone United ni timu ya aina gani? Yanga ina sura ipi kuelekea mechi hiyo? Makala haya yanachambua zikiwa zimebaki saa chache kuelekea mchezo huo.

Kwanza, Yanga wanakwenda kukutana na mabingwa mara tisa wa Ligi Kuu ya Botswana, ikiwamo misimu miwili mfululizo iliyopita [2024-25 na 2025-26]. Yanga wao ni mabingwa wa Ligi Kuu Bara kwa misimu mitano mfululizo.

Msimu uliopita, Gaborone United walitwaa ubingwa wao wa Ligi wakiwa wameshinda mechi 23, sare tano na kufungwa mara mbili pekee, wakimaliza na pointi 74.

Pili, Gaborone United si timu yenye ukubwa kwenye michuano ya Ligi ya Mabingwa kwani imeshiriki michuano hiyo mara mbili pekee na haikuweza kufika walau hatua ya makundi.

Tatu, Yanga haijaishia hatua hizi za awali kwa misimu mingi ya hivi karibuni, ikiwamo mitatu mfululizo iliyopita, na badala yake imekuwa ikipigia hesabu robo fainali au zaidi ya hapo.

Nne, kwa msimu huu [2026-27], Gaborone wamecheza mechi moja pekee ya Ligi Kuu ya Botswana, ambapo wakiwa nyumbani walipata ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Prisons XI.

Tano, hiki ni kipimo cha kwanza kwa kocha Manqoba Mngqithi katika ngazi ya michuano ya kimataifa akiwa na Yanga baada ya kufanya makubwa akiwa na Mamelodi, ambapo aliwahi kuipa taji hilo miaka mingi iliyopita.

Sita, wakati huu Ligi ya Botswana ikiwa katika raundi yake ya kwanza, ingawa baadhi ya timu bado hazijacheza hata mechi moja, Gaborone wako nafasi ya tatu kwenye msimamo, wakizidiwa kwa idadi ya mabao na Nico United iliyoko kileleni.

Saba, Gaborone ni timu inayoruhusu mabao. Katika mechi zilizopita, ni mbili pekee walioondoka uwanjani bila nyavu zao kutikiswa. Yanga wao wameruhusu mabao mawili pekee katika mechi tano zilizopita.

Nane, Gaborone wana rekodi nzuri wanapokuwa nyumbani. Wameshinda mechi zote nne zilizopita, wakizifunga Polisi [2-1], BDF XI [2-1], Calendar Stars [5-0], na Orapa United [6-1].

Related articles

Recent articles