22.9 C
New York

JET yawapiga msasa wahariri kuhusu migongano ya binadamu na wanyamapori

Published:

Na Mwandishi Wetu, Gazetini

Chama cha Waandishi wa Habari za Mazingira Tanzania (JET) kilifanya mafunzo maalum Septemba 5-6, 2024 kwa wahariri zaidi ya 20 huko Bagamoyo, Pwani, juu ya namna bora ya kuripoti migongano baina ya binadamu na wanyamapori.

Wahariri kutoka vyombo vya habari mbalimbali nchini wakiwa katika picha ya pamoja na wawezeshaji wa mafunzo kutoka JET na GIZ.

Mafunzo haya yaliandaliwa kwa lengo la kuongeza uelewa wa wahariri juu ya masuala ya uhifadhi na mazingira, ili kuwawezesha kuripoti kwa tija na kusaidia kupunguza migogoro hiyo kupitia vyombo vya habari.

Mafunzo haya yalifadhiliwa na Mradi wa Kupunguza Migongano Baina ya Binadamu na Wanyamapori Tanzania, unaotekelezwa na Shirika la Maendeleo la Ujerumani (GIZ), kwa niaba ya Serikali ya Ujerumani na kwa ufadhili wa BMZ.

Wataalamu wa mazingira na uhifadhi, wakiwemo maafisa wa Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA), walitoa elimu ya kina kuhusu mikakati ya kukabiliana na changamoto hiyo.

Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), Deudatus Balile, aliyeshiriki mafunzo hayo, alieleza kuwa uelewa wa masuala haya ni muhimu kwa waandishi na wahariri ili waweze kusaidia katika juhudi za kupunguza migongano.

Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) Deudatus Balile;

Balile aliwataka wataalamu wa uhifadhi kupewa nafasi kwenye vyombo vya habari ili kutoa majibu sahihi na elimu kwa jamii.

Isack Chamba, Ofisa wa TAWA, alieleza kuwa TAWA imekuwa ikichukua hatua mbalimbali kama kuua wanyamapori waharibifu 221 na kuhamisha wanyama 60, ikiwemo simba na chui, katika jitihada za kuhakikisha usalama wa binadamu. Hii ni sehemu ya juhudi za kupunguza migongano kati ya wakazi na wanyamapori katika maeneo yanayozunguka hifadhi.

Chamba pia alieleza changamoto za kuongezeka kwa shughuli za kibinadamu, kama kilimo na ufugaji, ambazo zinachangia migongano kati ya wakulima na wanyamapori, hasa katika maeneo ya Tunduru, Liwale, na Serengeti. TAWA imeendelea kutoa elimu kwa jamii juu ya namna bora ya kujikinga na madhara ya wanyamapori.

Mwenyekiti wa JET, Dk. Ellen Otaru, alisisitiza kuwa waandishi wa habari wana nafasi kubwa ya kusaidia kupunguza migongano hii kwa kutoa taarifa sahihi na kuelimisha umma. Mradi huu unatekelezwa hasa katika Ukanda wa Ruvuma na Lindi.

Related articles

spot_img

Recent articles

spot_img