NEW YORK, Marekani
RAIS wa Venezuela, Nicolás Maduro, aliyekamatwa katika operesheni ya kijeshi ya Marekani, amefikishwa katika mahakama ya Manhattan, New York, ambako leo Jumatatu Januari 5, 2026, atasomewa mashtaka yanayomkabili.
Maduro anatuhumiwa na Marekani kwa kujihusisha na biashara haramu ya dawa za kulevya, makosa yanayohusiana na silaha pamoja na kuendesha kile kinachoelezwa kama utawala wa “kigaidi wa dawa za kulevya,” madai ambayo amekuwa akiyakana vikali.
Katika operesheni hiyo hiyo, mke wa Maduro, Cilia Flores, naye alikamatwa na anakabiliwa na tuhuma za rushwa.
Hatua ya Marekani imekosolewa na washirika wa karibu wa Maduro, akiwemo China na Iran, ambao wanaitaka Washington kumuachilia huru mara moja. Serikali ya China, kupitia Beijing, imesema hatua hiyo ni “ukiukaji wa wazi wa sheria za kimataifa.”


