21 C
New York

Infographic| Tanzania ilivyonufaika na Trilioni 1.3

Published:

Kwa sasa unaweza kusema ni kama vyuma vimeachia! Hii ni kutokana na miradi yenye thamani ya Sh trilioni 1.3 itakayotekelezwa na Serikali ya Rais Samia Suluhu Hassan inatarajiwa kulegeza ugumu wa maisha uliodumu mitaani kwa miaka sita sasa.

Neema hiyo ya ‘kujazwa pesa’ haitaishia kwa wakandarasi na wafanyabiashara wakubwa pekee, bali itabisha hodi kwa akina mama ntilie, maelfu ya vijana wanaoranda mjini na vijijini kwa kukosa ajila. Haueni pia haitawasahau wamachinga.

Iko hivi; Oktoba 10, mwaka huu, Serikali ya Rais Samia imetangaza ‘kuachia’ Sh trilioni 1.3 za kutekeleza miradi mbalimbali nchini, fedha ambazo ni mkopo nafuu kutoka Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF).

Mkopo huo ulitolewa kwa ajili ya kukabiliana na athari za UVIKO-19, kufuatia mazungumzo ya Rais Samia na Mkurugenzi Mtendaji wa IMF, Kristalina Georgieva yaliyofanyika Mei 3, mwaka huu, pia alipokutana na Mkurugenzi wa IMF Kanda ya Afrika, Abebe Selassie (Juni 29, mwaka huu).

Akifafanua zaidi kuhusu fedha hizo kwenye hafla ya kuzindua Mpango wa Maendeleo kwa Ustawi wa Taifa, Waziri wa Fedha na Mipango, Dk. Mwigulu Nchemba, amesema kufuatia mazungumzo hayo yaliyokuwa na ufanisi kati ya Serikali na IMF, Septeba 7, mwaka huu Bodi ya Wakurugenzi wa Shirika hilo iliridhia mkopo nafuu kwa Tanzania wa jumla ya Dola za Marekani milioni 567.25, sawa na Sh trilioni 1.3 kwa ajili ya kukabiliana na athari za UVIKO-19.

 

“Fedha hizo zinajumuisha mkopo nafuu usio na riba kupitia dirisha la Rapid Credit Facility (RCF) wa jumla ya Dola za Marekani milioni 189.08 (sawa na theluthi moja ya mkopo wote); na mkopo nafuu wenye riba ndogo (asilimia 1.05) kupitia dirisha la Rapid Financing Instrument (RFI) wa dola za Marekani milioni 378.17 (sawa na theluthi mbili ya mkopo wote).

“Hivyo, fedha hizi ni za dharura na hivyo zitatakiwa kutumika ndani ya mwaka huu wa fedha (2021/22),” amesema Dk. Nchemba.

Miradi inayotekelezwa

Kwa mujibu wa Dk. Nchemba, miradi itakayotekelezwa ambayo ndiyo itakuwa kichocheo cha maendeleo kila kona ya nchi ni pamoja na ujenzi wa madarasa mapya 15,000 ya sekondari, madarasa 3,000 ya shule za msingi na kutengeneza madawati 462,795. Kwa mantiki hiyo, mafundi wa ujenzi, mafundi seremala watanufaika na mradi huu mkubwa wa aina yake na kwanza kwa Rais Samia.

“Jambo jingine ni kumalizia vyuo vya VETA 32, ununuaji wa magari 25 ya kuchimba visima vya maji na mitambo mitano ya kujenga mabwawa ya maji,” amesema Dk. Mwigulu.

“Katika eneo la afya, tunaenda kujenga ICU 72, kununua magari ya wagongwa (Ambulance) 375 na ya chanjo 214. Pia, mifumo ya Oksijen hospitali 82 na mitungi ya gesi 4,640,” amesema Dk. Nchemba.

Kwa mujibuwa Dk. Nchemba miradi mingine kwenye sektya afya ni pamoja na ununuzi wa mitambo ya kuzalisha hewa ya Oksijeni 40 na vitanda vya wagonjwa 2,700.

“Tukwenda kununua X-ray za kisasa 85, mashine za CT- Scan 29 na MRI kwa hospitali zote za kanda,”amesema Dk. Nchemba.

Related articles

spot_img

Recent articles

spot_img