3.9 C
New York

Dunia yaadhimisha Siku ya UKIMWI kwa onyo kali na wito wa kuchukua hatua

Published:

Na Mwandishi Wetu, Gazetini

Dunia leo Desemba 1, 2025, inaadhimisha Siku ya UKIMWI Duniani, huku Umoja wa Mataifa ukitoa onyo kali kuhusu mustakabali wa mapambano dhidi ya VVU na UKIMWI, sambamba na wito wa kuchukua hatua madhubuti. Kaulimbiu ya mwaka huu, “Kukabili misukosuko, kubadili mwelekeo wa hatua za UKIMWI,” inaelezwa kuwa ni mwito muhimu katika kipindi ambacho dunia iko katika hatua ya maamuzi ya kihistoria.

Katika ujumbe wake maalum, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, António Guterres, amesema kuwa japokuwa kumekuwa na hatua kubwa katika kupunguza maambukizi na vifo, mafanikio hayo yako hatarini kuporomoka.

“Maendeleo tuliyopata hayawezi kukanushwa. Tangu mwaka 2010, maambukizi mapya yameshuka kwa asilimia 40, na vifo vitokanavyo na UKIMWI vimeshuka zaidi ya nusu. Fursa ya kupata matibabu pia imeimarika,” amesema.

Hata hivyo, Guterres amesisitiza kuwa mamilioni ya watu bado wanaachwa nyuma kutokana na ukosefu wa usawa, unyanyapaa na mazingira wanamoishi.

“Mamilioni bado hawapati huduma za kinga na matibabu kwa sababu ya wao ni kina nani, wanaishi wapi, au unyanyapaa wanaokumbana nao,” ameeleza, akionya kuwa kupungua kwa ufadhili na kuongezeka kwa sheria kandamizi kunaweka hatarini mafanikio yaliyopatikana kwa miongo kadhaa.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa UNAIDS, Winnie Byanyima, amesema mwaka 2025 umekuja na mgogoro mkubwa wa ufadhili unaotishia kuyumbisha mafanikio yaliyofikiwa kwa juhudi kubwa. Ameitaka dunia kuchagua mabadiliko na kuendelea kusonga mbele badala ya kurudi nyuma.

“Kwa pamoja, bado tunaweza kumaliza UKIMWI ifikapo 2030 tukichukua hatua kwa haraka, kwa umoja na kwa kujitolea kusikoyumba,” amesema Byanyima.

Ameongeza kuwa mashirika yanayoongozwa na jamii-ambayo ndiyo nguzo katika kufikia makundi yaliyo pembezoni—ndiyo yanayoumia zaidi kutokana na kupungua kwa ufadhili. Aidha, sheria kandamizi zinazuia watu kupata huduma muhimu wakati ambapo zinahitajika zaidi.

“Uongozi wa kisiasa ni muhimu. Tunahitaji suluhu za kubadilisha mifumo, kuondoa unyanyapaa na ubaguzi, na kulinda haki za wanawake, wasichana na watu wa LGBTQ+,” amesisitiza.

Licha ya changamoto zinazoendelea, viongozi hao wanasema dirisha la kumaliza janga la UKIMWI bado liko wazi, iwapo kutakuwa na uwekezaji mpya na mshikamano wa kimataifa.

“Kumaliza UKIMWI kama tishio la kiafya kufikia 2030 kunawezekana. Hebu tukamilishe kazi hii,” umehitimisha ujumbe huo.

Maadhimisho haya yanakumbusha kuwa dunia ina uwezo na nyenzo za kutokomeza UKIMWI—ikiwa tu itaamua kuzitumia kikamilifu.

Related articles

spot_img

Recent articles

spot_img