Na Mwandishi Wetu, Gazetini
Wachezaji wa timu ya Gor Mahia nchini Kenya wameeleza jinsi walivyopokea kwa uchungu mkubwa kifo cha Waziri wa zamani wa Kenya, Raila Odinga ambaye ni mlezi wa klabu hiyo, aliyefariki nchini India alipokuwa anapatiwa matibabu.
Katika kurasa za kijamii za Gor Mahia, klabu imetoa salamu za rambirambi, huku baadhi ya wachezaji wake wakimzungumzia kiongozi huyo aliyekuwa shabiki mkubwa wa timu hiyo.

Baadhi ya nyota timu hiyo akiwamo Nahodha Philemon Otieno, wamezungumzia walivyopokea taarifa ya kifo cha kiongozi huyo, kuwa ni huzuni kubwa kwao kumpoteza mlezi wao ambaye alikuwa karibu katika kuisapoti klabu.
Otieno amesema, Hayati Ondinga alikuwa mlezi wa klabu hiyo kwa muda mrefu na walimchukulia ni kama baba yao na mshauri katika mambo mbalimbali.
“Tuna huzuni sana kumpoteza mlezi wetu, ukizingatia hatukujiandaa kupokea taarifa kama hiyo,” amesema Nahodha Msaidizi wa klabu hiyo, Geoffrey Ochieng kupitia GOR TV.
“Taarifa nimepokea kwa uchungu sana, imekuja kipindi tunajiandaa kwenda mazoezi na hata katika mazoezi morali ilikuwa chini sana na kocha akajaribu kuongea na sisi. Nakumbuka derby yangu ya kwanza alitupigia simu kwanza akasema anakuja uwanjani na tusimuangushe,” amesema beki Joshua Onyango.
Wakati wa uhai wake, Odinga ameisaidia klabu hiyo katika mambo mbalimbali kuhakikisha inafanya vizuri katika mashindano na mwanzoni mwa mwezi huu, aliahidi kutoa kiasi cha fedha Shilingi milioni 10 za Kenya kwa ajili ya kusaidia shughuli za kiutawala za klabu katika msimu wa 2025/2026.


