9.3 C
New York

Yanga v FAR Rabat; Rekodi zinabana, zinaachia

Published:

Na Hassan Mwasha, Gazetini
YANGA watashuka dimbani wikiendi hii (Novemba 22) kwa mchezo wao wa kwanza wa hatua ya makundi msimu huu wa Ligi ya Mabingwa Afrika.
Ni katika Uwanja wa New Aman Complex, ambapo watakuwa wenyeji wa FA Rabat ya Morocco katika mchezo huo wa Kundi B. Rekodi zinasemaje?
FAR Rabat hawapoi ugenini
FAR Rabat imefungwa mechi moja pekee kati ya tano za Ligi ya Mabingwa ilizocheza ugenini hivi karibuni.
Katika mechi hizo, timu hiyo ya Ligi Kuu nchini Morocco ilikutana na Horoya, Real Banjul, Pyramids, Mamelodi Sundowns na Maniema.
Iko hivi; mchezo waliopoteza ni dhidi ya Pyramid ya Misri, ambao ulimazika kwa FAR Rabat kutandikwa mabao 4-1 mjini Cairo.
Itakumbukwa, mechi waliyoshinda ugenini kati ya hizo tano ni ile ya ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Banjul ya Gambia.
Michezo mitatu iliyobaki walitoa sare ya bao 1-1 dhidi ya Horoya (Guinea), Mamelodi (Afrika Kusini) na Maniema (DRC).
Yanga wakiwa nyumbani
Hata hivyo, wakati rekodi za ugenini zikionekana kuibeba FAR Rabat, bado zinawabana Waarabu hao wa Afrika ya Kaskazini. Wanakutana na Yanga, ambayo pia ni tishio inapokuwa nyumbani.
Wakiwa katika ardhi ya nyumbani kwenye mechi tano za Ligi ya Mabingwa walizocheza hivi karibuni, Yanga walikutana na Silver Strikers, Wiliete SC, MC Alger, TP Mazembe na Al Hilal.
Katika mechi hizo, mabingwa hao wa Ligi Kuu Bara walishinda tatu, wakizifunga Strikers (2-0), Wiliete (2-0) na TP Mazembe (3-1).
Mchezo pekee waliopoteza wakiwa mbele ya mashabiki wao ni ule wa kichapo cha mabao 2-0 kutoka kwa Al Hilal ya Sudan, pia wakilazimishwa suluhu (0-0) na MC Alger ya Algeria.
Yanga wafanye nini?
Uzoefu wa soka la Afrika, ikiwamo michuano hii ya Ligi ya Ligi ya Mabingwa, unaonesha kuwa timu zinazofanikiwa zaidi ni zile zenye uwezo wa kupata matokeo mazuri katika mechi zake za nyumbani.
Wachezaji wa Yanga wanapaswa kujitoa katika kila sekunde ya dakika 90 za mchezo huo kwa kuzipambania pointi tatu za nyumbani. Hilo litawezekana vipi?
Kubwa ni nidhamu ya mchezo. Si tu kuwaheshimu wapinzani, bali pia kila mchezaji kutekeleza kwa asilimia 100 majukumu yake ndani ya uwanja.
Mathalan, dhidi ya timu za daraja la FA Rabat, ni ngumu kutarajia nafasi nyingi za kufunga. Hivyo, washambuliaji wa Yanga wawe na nidhamu ya hali ya juu katika kutumia nafasi chache zitakazojitokeza kupata mabao.
Kwa upande mwingine, angalizo kwa safu ya ulinzi ya Yanga ni ubora mkubwa wa timu za Afrika ya Kaskazini, ikiwamo FAR Rabat, katika kutumia mipira ya vichwa inayotokana na faulo, kona au krosi.
Iko wazi, kwamba mabeki wa Yanga wamekuwa na changamoto hiyo ya kucheza mipira ya vichwa. Ni bahati kwao kwani timu imekuwa ikishinda, hivyo udhaifu huo kutokupata nafasi ya kuzua mijadala.

Related articles

spot_img

Recent articles

spot_img