Na Mwandishi Wetu
Katibu wa Jumuiya na Taasisi za Kiislam Tanzania, Sheikh Ponda Issa Ponda, leo Alhamisi Juni 5, 2025, ametangaza kujiunga na Chama cha ACT-Wazaendo, katika hafla iliyofanyika Magomeni, jijini Dar es Salaam.
Sheikh Ponda, ametangaza uamuzi wake wa kujiunga na ACT Wazalendo mbele ya umati wa wafuasi na viongozi wa chama hicho, huku akisema lengo ni kuhakikisha utawala wa sheria,uchaguzi huru na wa haki unapatikana.

Amesema ameona umuhimu wakuunga mkono oparesheni ya ACT Wazalendo ya ‘Linda Demokrasia’, akisisitiza kuwa Taifa lolote linastahili kuongozwa katika misingi ya sheria kwa kila mtu bila kujali cheo wala kabila.
Aidha ametoa wito kwa vijana, wanawake, wazee, na viongozi wa dini kuungana katika uwanja wa mapambano ya kudai haki mbalimbali zikiwemo za kisiasa kama vile kuhakikisha kura zetu zinahesabiwa kwa haki na viongozi wanaochaguliwa na wanawakilisha matakwa ya wananchi.
‘Kwa hiyo ndugu zangu mimi nimeamua kujiunga ACT Wazalendo sio kwa sababu tu za kisiasa, mimi nimeamua kujiunga nikiamini kwamba katika jukwaa hili ule uhuru wa kufanya zile harakati za kupambania haki za wanadamu unapatikana,” amesema Sheik Ponda.



