Na Mwandishi Wetu
Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Makonda ameomba sh. 525.32 bilioni kwa bajeti ya wizara hiyo kwa mwaka wa fedha 2026/27 kwa ajili ya kutekeleza vipaumbele tisa.
Akiwasilisha bajeti ya Wizara hiyo leo Mei 4, 2026, bungeni jijini Dodoma, ametaja miongoni mwa vipaumbele hivyo ni kukamilisha ukarabati, uboreshaji na ujenzi wa miundombinu, kukamilisha maandalizi ya Michuano ya Mataifa ya Afrika (AFCON 2027).
Vingine ni maandalizi ya kuwa mwenyeji wa Mashindano ya 74 ya Urembo ya Dunia (Miss World), kukamilisha utungaji na uhuishaji wa sera, sheria, mikakati, miongozo na kanuni mbalimbali ili kuimarisha usimamizi na utekelezaji wa majukumu katika sekta hizo.

Pia kuimarisha ushiriki wa timu za Taifa katika mashindano ya kimataifa, kuboresha elimu na mafunzo katika tasnia za utamaduni, sanaa na michezo, pamoja na kuratibu na kusimamia matamasha, shughuli na matukio makubwa.
Katika hatua nyingine Makonda ameelezea maandalizi ya miundombinu kwa ajili ya AFCON 2027, kuwa tayari yamefikia hatua za ukamilishaji katika miji wenyeji, ikiwa ni sehemu ya kuhakikisha Tanzania inakuwa mwenyeji bora wa mashindano hayo makubwa barani Afrika.
Makonda amesema ukarabati wa Uwanja wa Benjamin Mkapa umefikia asilimia 95, huku viwanja vitatu vya mazoezi vya Gymkhana, Meja Jenerali Isamuhyo na Shule ya Sheria vikiwa tayari vimekamilika.
Aidha, ujenzi wa viwanja vingine vya mazoezi vya Farasi, Leaders Club na Gymkhana II unaendelea katika hatua za awali.
Kwa upande wa Arusha, ujenzi wa uwanja mkubwa wenye uwezo wa kuchukua watazamaji 32,000 umefikia asilimia 77.5, huku kiwanja kimoja cha mazoezi ndani ya eneo hilo kikiwa kimefikia asilimia 60.
Waziri Makonda amesema Serikali ina matumaini kuwa ifikapo Agosti 2026, miundombinu yote muhimu kwa ajili ya AFCON 2027 itakuwa imekamilika, hatua itakayoiwezesha Tanzania kuandaa mashindano hayo kwa viwango vya kimataifa na kuvutia wageni kutoka mataifa mbalimbali.


