Na Mwandishi Wetu
Nyota wa Yanga, Allan Okello amewahakikishia mashabiki wa timu hiyo kuwa watamaliza kila kitu ndani ya dakika 90 katika mchezo wa hatua ya 16 bora ya kombe la shirikisho dhidi ya TMA Stars utakaopigwa kesho kwenye dimba la KMC Complex, jijini Dar es Salaam.
Akizungumza na waandishi wa habari leo Aprili 10, Okello amesema wapinzani wao hawana cha kupoteza lakini upande wa Yanga wakipoteza itakuwa ni habari kubwa zaidi, hivyo kuwataka wachezaji wenzake kuzingatia maelekezo ya mwalimu.
“Nina matumaini makubwa kama tutaendelea na morali ya mchezo uliopita basi tutapata ushindi wa kishindo. Wachezaji tunapaswa kuwa watulivu uwanjani na kufuata maelekezo ya waalimu wetu. Ukifanya kosa moja tu kwenye mchezo wa mtoano inaweza kubadilish historia. Hii sio ligi. Ninawahakikishia wananchi kuwa tutamaliza kila kitu ndani ya dakika 90”
Hata hivyo ameeleza kuwa hawabezi wapinzani wao, kwani mpira unahitaji kuwa na heshima kwa kila mpinzani, bali ni wajibu wa kila mchezaji wa kuzingatia malengo yao na kutumia nguvu ile ile wanayotumia katika Ligi Kuu.


