5.7 C
New York

Mashabiki Simba kulipa faini ya CAF

Published:

Na Winfrida Mtoi, Gazetini

KLABU ya Simba imewatangazia wanachama na mashabiki wa timu hiyo namba maalumu za  kuchangia fedha kwa ajili ya kusaidia kulipa  faini waliyopigwa na Shirikisho la Soka Afrika(CAF) kutokana na matukio  waliyofanya  katika mechi za Kombe la Shirikisho Afrika msimu uliopita.

Simba imepewa adhabu ya kulipa faini ya jumla ya Dola 85,000 ambazo ni zaidi ya Sh 200 milioni. Faini ya awali ni Dola 50,000 (takribani Sh 135 milioni), zilitokana na vurugu zilizofanyika pamoja kuwasha fataki kwenye mchezo dhidi ya Al Masry ya Misri kwenye Uwanja wa Benjamini Mkapa, Dar es Salaam.

Adhabu hiyo ni pamoja na kucheza bila mashabiki katika mchezo wao wa  Ligi ya Mabingwa msimu huu dhidi ya Gaborone United kutoka Botswana, utakaopigwa Septemba 28,2025  kwenye uwanja huo.

Pia Simba imepewa adhabu nyingine ya faini ya Dola 35,000 (sawa na Sh 78 milioni) kutokana na makosa ambayo ilifanya katika mchezo wa marudiano wa Kombe la Shirikisho Afrika dhidi ya RS Berkane, Mei 25, mwaka huu.

Meneja Habari na Mawasiliano wa Simba, Ahmed Ally amethibitisha hilo leo Ijumaa Septemba 26, 2025 wakati akizungumza na waandishi wa habari  kuwa wamepokea barua kutoka CAF  ya kutorusu mashabiki kuingia uwanjani katika mechi yao na Gaborone.


“Nipo hapa kuwathibitishia kwamba mechi yetu ya Jumapili haitakuwa na mashabiki kutumikia adhabu ya CAF. Kilichosababisha ni mchezo ni dhidi ya Al Masry, kuna shabiki aliingia uwanjani na kuna mashabiki waliwasha moto. 

“Kwa hiyo kama mtu anataka kulipa faini yote kwa ajili ya kuisaidia klabu namba za Lipa Namba zipo. Inawezekana wewe  ulipanga kwenda kwenye mechi tarehe 28, kile kiingilio change ulichopanga kulipa, tuwekee kwenye Lipa Namba twende tukalipe faini ya CAF. Nataka tushirikiane chini ya kampeni yetu ya Letu Sote,” amesema Ahmed.

Aidha amewaasa mashabiki wa timu hiyo, kuacha tabia ya kufanya vitendo vinavyoigharimu tena klabu hiyo.

“Niwaase mashabiki wenzangu wa Simba, uache vitendo vya vurugu uwanjani. Kwanza tuanze ulinzi wa wenyewe kwa wenyewe ukiona mtu anataka kuwasha zile fireworks mzuie, ukiona mtu anataka kuingia uwanjani tushirikiane kumzuia ikiwezekana kumtoa uwanjani. Angalia mechi kama hii tunakwenda uwanjani bila mashabiki,”

Related articles

spot_img

Recent articles

spot_img