13.1 C
New York

Rais Mwinyi aipongeza Yanga, aizawadia  milioni 100

Published:

Na Mwandishi Wetu

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi ameizawadia Klabu ya Yanga  Sh 100 milioni  kwa kutambua ushindi na mafanikio makubwa waliopata katika msimu wa mwaka 2024/2025.

Rais  Mwinyi ameyasema hayo leo Juni 30, 2025 alipokutana na viongozi pamoja na wachezaji wa Yanga waliofika Ikulu  Zanzibar kwa ajili ya kumkabidhi makombe matano ya michuano mbalimbali waliyoyatwaa msimu huu.

Amepongeza mafanikio hayo makubwa yaliyopatikana na klabu hiyo kongwe, akieleza kuwa yanajenga heshima na historia muhimu katika tasnia ya michezo nchini.

Aidha, ameishukuru klabu hiyo  kwa kuendelea kuitangaza Zanzibar ndani na nje ya nchi kupitia kampeni ya Visit Zanzibar, huku akieleza kuwa hatua ya klabu hiyo kucheza baadhi ya michezo yake Zanzibar kunachangia kukuza uchumi na sekta ya utalii kutokana na kuongezeka kwa idadi ya wageni na wananchi kunufaika na fursa mbalimbali.

Halikadhalika, Rais Mwinyi amesema Serikali itaendelea kuimarisha viwanja vya michezo ili kuwezesha michuano mingi zaidi kufanyika Zanzibar.

Naye Rais wa Yanga ambaye pia ni Mwenyekiti wa Vilabu vya Soka Barani Afrika, Hersi Said, amemkabidhi Rais Mwinyi medali maalum ya michuano ya CRDB  pamoja na jezi ya ubingwa wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara na kutoa pongezi na shukrani kwa Rais  kutokana na  juhudi zake za kuimarisha miundombinu ya michezo nchini na kuahidi kuwa klabu hiyo itaendelea kucheza mechi zake visiwani humo.

Katika msimu wa 2024/2025 Yanga  imefanikiwa kutwaa makombe  matano ambayo ni Ngao ya Jamii, Kombe la Michuano ya Toyota, Kombe la Muungano, Kombe la Ligi Kuu  Tanzania Bara na Kombe la Shirikisho.

Related articles

spot_img

Recent articles

spot_img