2.9 C
New York

WHO: Dunia imeshindwa ukomesha ukatili dhidi ya wanawake

Published:

Na Mwandishi Wetu, Gazetini

SHIRIKA la Afya Duniani (WHO) likishirikiana na wadau wa Umoja wa Mataifa limetoa ripoti muhimu leo jijini Geneva, Uswisi, ikibainisha kuwa ukatili dhidi ya wanawake bado ni miongoni mwa ukiukwaji mkubwa zaidi wa haki za binadamu, huku takwimu za zaidi ya miaka 20 zikionesha kutokuwepo kwa maendeleo makubwa katika kupunguza tatizo hilo.

Ripoti hiyo imechanganua data za kimataifa kuhusu mateso, manyanyaso na ukatili wa kijinsia dhidi ya wanawake, ikionesha ukubwa wa changamoto inayodhoofisha usalama, afya na utu wa mamilioni ya wanawake duniani.

Kwa mujibu wa takwimu, mwanamke 1 kati ya 3 duniani-zaidi ya milioni 840-ameteseka kutokana na ukatili wa kimapenzi au kijinsia kutoka kwa mwenzi wake tangu mwaka 2000, kiwango ambacho hakijabadilika kwa miongo miwili. Katika mwaka uliopita pekee, wanawake milioni 316 (asilimia 11) walipitia ukatili wa wenzi wa karibu, huku milioni 263 wakiripotiwa kukumbana na ukatili wa kingono kutoka kwa watu wasiokuwa wenzi tangu wakiwa na umri wa miaka 15.

Mkurugenzi Mkuu wa WHO, Dkt. Tedros Adhanom Ghebreyesus, amesema ukatili dhidi ya wanawake umeendelea kuwa dhuluma yenye mizizi mikubwa katika jamii, akisisitiza kuwa hakuna taifa linaloweza kujiona salama wakati nusu ya watu wake wanaishi kwa hofu.

Ufadhili mdogo, mahitaji makubwa

Ripoti inatolewa wakati dunia inajiandaa kuadhimisha Siku ya Kimataifa ya Kutokomeza Ukatili Dhidi ya Wanawake (Novemba 25), ikionyesha kuwa licha ya kuwepo mikakati inayothibitishwa, ufadhili wa kimataifa unapungua. Mwaka 2022, programu za kuzuia ukatili zilipokea asilimia 0.2 tu ya fedha za maendeleo—kiasi ambacho kimeendelea kupungua hadi mwaka 2025.

Hatari pana kwa wanawake na wasichana

Ripoti inabainisha kuwa ukatili mara nyingi huanza mapema. Wasichana balehe milioni 12.5 (16% ya wenye umri wa miaka 15–19) walipitia ukatili kutoka kwa wenzi wao katika mwaka mmoja uliopita. Athari zake zinahusisha mimba zisizotarajiwa, magonjwa ya zinaa na msongo wa mawazo.

Tatizo hili ni kubwa zaidi katika nchi maskini au zenye migogoro. Eneo la Oceania (bila Australia na New Zealand) lina kiwango cha juu zaidi duniani—asilimia 38—zaidi ya mara tatu ya wastani wa kimataifa.

Wito wa hatua za haraka

Ripoti inazitaka serikali na jumuiya ya kimataifa kuongeza ufadhili na kuchukua hatua madhubuti kwa: Kukuza programu za kuzuia ukatili kwa ushahidi wa kitaalamu; Kuimarisha huduma za afya, sheria na msaada wa kijamii kwa manusura; Kuwekeza kwenye mifumo ya ukusanyaji data; Kutekeleza sheria na sera zinazowawezesha wanawake na wasichana

Ripoti imetolewa sambamba na toleo jipya la mfumo wa RESPECT Women, linalotoa mwongozo wa kuzuia ukatili hata katika mazingira ya dharura. Inasisitiza kuwa huu si wakati wa ukimya-ni wakati wa hatua thabiti za kulinda maisha na hadhi ya wanawake na wasichana duniani.

Related articles

spot_img

Recent articles

spot_img