Na Mwandishi Wetu
WATU wawili wamejeruhiwa kutokana na ajali ya moto iliyotokea leo Januari 16,2025 katika jengo la NSSF lililopo katika mtaa wa Azikiwe na Samora, Posta,Dar es Salaam.
Akizungumza na waandishi wa habari baada ya zoezi la uokoaji Mkaguzi Msaidizi wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji Ilala, Frank Mwalongo amethibitisha kujeruhiwa kwa watu hao wawili ambao wamewahishwa hospitali ya Mnazi Mmoja kwa huduma ya kwanza.
“Majira ya saa sita na robo mchana tulipokea wito wa dharura kuhusu ajali ya moto katika jengo la NSSF, na walifanikiwa kufika eneo la tukio kwa wakati na kuweza kupambana na moto huo na kuudhibiti,” amesema.

Ameeleza kuwa ajali hiyo haijaleta madhara makubwa kwa jengo ambapo ghorofa ya kwanza ya jingo ndiyo imeathirika kidogo, lakini mali zimeokolewa na watu wote walikuwemo ndani wako salama.
Mwalongo amesema bado chanzo cha moto huo hakijajulikana, uchunguzi unaendelea na ukikamilika taarifa rasmi itatolewa.


