21 C
New York

Chart| Tembo wanavyoitesa Serikali Same

Published:

*Wadau wasema utafiti wa kina unahitajika ili kupata suluhu

Na Jackline Jerome, Gazetini

Vijiji 25 wilayani Same mkoani Kilimanjaro Kaskazini mwa Tanzania yamegauka kuwa maskani ya wanyama Tembo. Hatari kubwa ni kwamba tembo hao wamekuwa wakiharibu ekari za mazao ya chakula.

Takwimu kutoka ndani ya Wilaya ya Same zinaonyesha kuwa jumla ya ekari 3,534.55 za mazao ya chakula zimeharibiwa na tembo ndani ya miaka 10 kuanzia mwaka 2014 hadi Juni 2023.

Hatua hiyo imeilazimu Serikali kutumia njia ya Helkopita kwa ajili ya kuwasaka na kuwadhibiti tembo hao waliozagaa katika vijiji hivyo 25 vya Wilaya ya Same na kuwavisha vifaa maalum vya mawasiliano kufuatilia mwenendo wao miongoni mwa njia za kudhibiti athari za mwingiliano wa shughuli za kibinadamu na Uhifadhi.

Zoezi hilo ni utekelezaji wa agizo la Waziri wa Maliasili na Utalii, Mohammed Mchengera alilotoa hivi karibuni alipofanya ziara ya kikazi ya siku moja katika wilaya hiyo ya Same ambapo ameagiza Mamlaka ya Hifadhi za Taifa (TANAPA) kupeleka Helkopita katika wilaya hiyo kusaidia zoezi la kuondoa makundi ya tembo yaliyozagaa katika maeneo mbalimbali na kuwarejesha katika maeneo ya hifadhini.

Oparesheni hiyo inatekelezwa kwa ushirikiano baina ya Taasisi nne zilizo chini ya wizara ya Maliasili na Utalii, Kamati ya Ulinzi na Usalama Wilaya ya Same na Wananchi wenyeji ambao wanasaidia kuainisha maeneo walipo tembo.

Mkuu wa hifadhi ya Taifa Mkomazi, Kamishna Msaidizi wa Uhifadhi, Emmanuel Moirana amesema kwa siku ya kwanza jumla ya makundi matano ya tembo yamerejeshwa hifadhini, mkakati uliopo ni kuendelea na zoezi hilo kuondoa changamoto ya mara kwa mara kuripotiwa makundi ya tembo kuonekana maeneo ya nje ya hifadhi.

Kwa upande wake mkuu wa Wilaya ya Same, Kasilda Mgeni amepongeza jitihada hizo za wizara uharaka wa kutekeleza ahadi ya kuondoa tembo hao kwa kuongeza vitendeakazi na rasilimali watu, akisema huenda changamato ikapungua na wananchi kuweza kuendelea na shughuli za uzalishaji.

“Baada ya kupata taarifa za ukubwa wa tatizo Mhe.Waziri aliagiza TANAPA kuleta Helkopta ndani ya siku mbili kusaidia katika oparesheni ya kuwajeshesha tembo kwenye maeneo ya hifadhi, kwakweli zoezi sio rahisi sana lakini tunamshukuru Mungu zoezi limefanyika kwa ufanisi mkubwa na wananchi wameonekana kufurahia kuona serikali yao ni sikivu,” amesema Kasilda Mgeni-Mkuu wa Wilaya ya Same.

Baadhi ya waazi wa wilaya ya Same walioshiriki katika oparesheni hiyo wamesema kuna idadi kubwa ya tembo ambao wametoka kbisa kwenye maeneo ya hifadhi na kufanya makazi ya kudumu kwenye maeneo ya vijiji, hali ambayo imesababisha baadhi yao hasa wakulima mwaka huu kukosa kabisa mazao.

“Madhara ya watu kuuliwa na Tembo kwa hapa kitongoji cha Kabambuu hayajatokea ni athari tu za mazao kuliwa na tembo yaani kunawatu hawatavuna kabisa hata chembe ya mahindi kupeleka nyumbani kwao hakuna na niwengi wameathirika,” amesema Sallum Omary Mwenyekiti wa Kitongoji cha Kavambuu kata ya Same Mjini.

Mwenendo wa uharibifu wa ekari za mazao wilayani Same mkoani Kilimanjaro kuanzia 2014

MWAKAEKARI ZILIZOHARIBIWA VIFO VYA WATU
201417
201522.5
201627
2017125
2018421.5
2019757.251
2020421.5
2021475.252
2022620.92
2023 hadi Juni1,121.91
JUMLA3,534.557

Taarifa iliyowasilishwa na Mkuu wa wilaya ya Same Kasilda Mgeni kwa waziri wa Maliasili na Utalii, Mohamed Mchengerwa Julai 5, 2023 zinaeleza kuwapo kwa ongezeko la matukio ya tembo kuvamia kwenye maeneo ya makazi mwaka hadi mwaka.

Wadau wanasemaje?

Mkurugenzi Mtendaji wa Chama cha Waandishi wa Habari za Mazingira Tanzania(JET), John Chikomo akizungumza na gazetini amesema tembo hao wanaweza kudhibitiwa iwapo Serikali itakamilisha mpango wake wa kuongoa korido ambao tayari imeuanza.

“Katika hili kama tunavyojua serikali tayari imeunda kamati ya mpango wa kuongoa korido hizi, lengo likiwa ni kutenganisha mapitio haya ya wanyama na binadamu, sisi wadau tunaona hii ni hatua nzuri sana kwani itasaidia kuondoa migogoro hii ya mara kwa mara ikiwamo uharibifu wa mazao.

John Chikomo.

“Sababu katika maeneo ambayo wananchi wanakaa jirani na hifadhi watu watasogezwa, mfano sehemu kama Bunju hakuwezi kuwa na migogoro sababu hakuna hifadhi tofauti na maeneo kama Saadan ambapo kuna hifadhi, hivyo kwa mtazamo wetu kama wadau wa mazingira mpango huu wa Serikali utasaidia kupunguza migogoro ya wanyama na binadamu.

“Jambo jingine ambalo tunaamini kwamba litafanikiwa ni hatua ya kutenga ardhi kwa ajili ya matumizi bora kwani eneo hili litakuwa la makazi na mambo mengine,” amesema Chikomo.

John Noronha ambaye ni Mtaalamu Mshauri wa kujitegemea wa masuala ya Mazingira ameiambia Gazetini kuwa ili Serikali iweze kudhibiti tembo hao wasiweze kurejea kuna hatua kadhaa za kufanya ikiwamo kuhisisha nchi ya Kenya.

John Noronha-Mtaalamu Mshauri wa kujitegemea wa masuala ya Mazingira. Picha| Gazetini

“Kwanza kabisa eneo lile la Same kuna Hifadhi ya Taifa ya Mkomazi, tembo wamekuwa wakizunguka sana eneo lile na hata wakati mwingine kuvuka na kuingia nchi jirani ya Kenya, hivyo kwa nyakati tofauti wamekuwa wakisababisha migogoro ya kibinadamu.

“Hivyo ili kuwadhibiti inatakiwa kwanza kufanyika kwa utafiti wa kina kuhusu wanyama hawa kwa maana ya muda wanaopita kwa maana ya vipindi(Tans Location) na kuona ni nyakati gani ambazo wanavamia zaidi kama ni kipindi cha mavuno au la,” amesema Noronha na kuongeza kuwa:

“Katika hili idara zinazohusika katika nchi zote mbili Tanzania na Kenya zinatakiwa kukutana na kuangalia mazingira ya kuwadhibiti tembo hawa kwani kwenye udhibiti wake kunahusisha gharama, lazima kwanza waangalie gharama zilizopo katika kuwafukuza.

“Hili linahusisha wadau wa maendeleo ili kupatikana uwezeshaji wa kuja na mwarobaini wa kudumu kwani kinyume na hivyo jambo hili litaendelea kujirudia na kuteza wananchi,” amesema John.

Related articles

spot_img

Recent articles

spot_img