23.5 C
New York

Sakata la dabi ya Kariakoo, Serikali yatoa msimamo

Published:

Na Mwandishi Wetu

Serikali imesema kuwa inaendelea kufuatilia kwa makini sakata la mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara kati ya Yanga na Simba, lakini haitangilia moja kwa moja kuepuka vikwazo vya FIFA huku ikisisitiza kanuni na sheria zilizowekwa za uendeshaji wa mpira zifuatwe.

Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Hamis Mwinjuma  ‘MwanaFA’ amesema hayo leo Juni 11 2025 Bungeni jijini Dodoma alipojibu swali la nyongeza la mbunge wa Makete, Festo Sanga.

“Tunafuatilia kwa ukaribu namna mgogoro unavyoendelea kutatulia huku tukijaribu kwa kiwango kikubwa kutoingilia maamuzi ya TFF na bodi ya ligi na tunasisitiza mamalaka kufuata kanuni na sheria walizojiwekea za Mpira wa miguu” amesema.

Katika hatua nyingine Serikali kwa kushirikiana na Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) imeandaa programu za kusimamia na kulea timu za Taifa za vijana walio na umri wa chini ya miaka 15 (U15), 17 (U17) na walio chini ya miaka 23 (U23) ili kuandaa timu ya Taifa ya wakubwa iliyo imara na madhubuti itakayoleta ushindani katika mashindano ya AFCON 2027.

Hayo yamesemwa bungeni Jijini Dodoma na  Mwana FA  alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Jimbo la Tunduru Kaskazini, Hassan Kungu aliyetaka kujua ni upi mkakati wa Serikali wa kuandaa timu ya Taifa madhubuti itakayowakilisha Taifa katika mashindano ya AFCON 2027, Tanzania ikiwa mwenyeji.

Amesema ipo mikakati mbalimbali ukiwemo wa kuimarisha ligi ya ndani kwa kuhakikisha ushindani na nidhamu ya michezo ili kuibua vipaji bora vya wachezaji wa ndani.

Aidha, amesema Serikali kwa kushirikiana na TFF itaendelea na mpango wa kufanya ‘scouting’ kwa wachezaji wa ‘diaspora’ katika mataifa mbalimbali duniani ambapo hadi sasa mpango huo umeonesha matokeo chanya kwa kujumuisha wachezaji hao kwenye mechi ambazo timu ya Taifa ya soka (Taifa Stars) ilifanya vizuri na kufanikiwa kufuzu kushiriki mashindano ya AFCON.

Mwana FA ameongeza kuwa Serikali inatambua Tanzania kuwa ni mwenyeji wa mashindano ya AFCON 2027 ambapo ametaja ni heshima kubwa na fursa ya kihistoria, hivyo Serikali imejipanga kuhakikisha Taifa Stars haishiriki tu bali inashindana kwa kiwango cha juu.

Related articles

spot_img

Recent articles

spot_img