Na Mwandishi Wetu, Gazetini
Viongozi mbalimbali na wakazi wa Mwanga na maeneo ya jirani kuaga mwili wa aliyewahi kuwa Makamu wa Kwanza wa Rais na Waziri Mkuu Tanzania, Hayati Cleopa Msuya kwenye Uwanja wa Cleopa Msuya uliopo wilayani Mwanga, mkoani Kilimanjaro.
Mwili wa Hayati Msuya aliyefariki Mei 7, 2025, jijini Dar es Salaam, uliwasili Mei 12, 2025 wilayani humo ukisindikizwa na msafara wa viongozi mbalimbali wa serikali, maafisa wa jeshi, pamoja na wanafamilia.


Akizungumza wakati wa kutoa salamu zake,Waziri Mkuu mstaafu Mizengo Pinda,amesema hayati Msuya alikuwa ni kiongozi aliyependa kusema ukweli hata katika mazingira magumu, huku akieleza kuwa kiongozi huyo atakumbukwa kwa mchango wake mkubwa katika kuleta maendeleo wilayani Mwanga, Mkoa wa Kilimanjaro na Taifa kwa ujumla.
Aidha, amewataka viongozi wa dini zote nchini kushikamana na kuliombea Taifa pamoja na viongozi wote wa Serikali ili wapate baraka na hekima kutoka kwa Mungu ya kuliongoza Taifa.

Baada ya kuagwa Mwanga, mwili wa Mzee Msuya utapelekwa nyumbani kwake Usangi kwa ajili ya maziko yatakayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan Jumanne Mei 13,2025.