Na Mwandishi Wetu
Katibu Mkuu wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Dk. John Jingu amesema Serikali inaendelea na juhudi mbalimbali kuhakikisha kwamba jamii inaamka na kuachana na ukatili wa kijinsia ambao umekua ni kikwazo cha maendeleo kwa ujumla.
Dk. Jingu ameyasema hayo Juni 11, 2025 jijini Dodoma alipokutana na Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Umoja wa Mataifa linalohusika na masuala ya Usawa wa Jinsia (UN Women), Hodan Addou kwa ajili ya kujadili utekelezaji wa afua mbalimbali nchini juu ya uwezeshaji wanawake kiuchumi.
Amesema Serikali imezingatia masuala ya usawa wa kijinsia katika nyanja mbalimbali ikiwa juhudi za Serikali katika kuleta usawa huo katika jamii.

“Kuna Kampeni ya Amsha Ari inayoendelea ambayo imelenga kujenga ufahamu juu ya masuala mbambali ya kimaendeleo kwa wananchi katika mikoa yote nchini ikiwemo suala zima la kuwainua wanawake kiuchumi,” amesema.
Aidha Dk. Jingu ameipongeza UN Women kwa kazi nzuri linalofanya katika kuunga mkono juhudi za Serikali ili kuleta usawa wa jinsia nchini na kuwaeleza kuwa wanaweza kuongeza nguvu katika kampeni hiyo ya mageuzi ya kifikra ya “Amsha Ari” ili kuweza kukuza usawa wa kijinsia nchini.
Kwa upande wake Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Umoja wa Mataifa linalohusika na masuala ya Usawa wa Jinsia (UN Women) Hodan Addou ameahidi kuwa Shirika hilo litaendelea kuunga mkono juhudi za Serikali katika kupunguza na ukatili wa kijinsia na kukuza usawa wa kijinsia.