Na Mwandishi Wetu
Jeshi la Polisi Mkoa wa Mwanza limesema linamshikilia na kumhoji Diana Bundala maarufu Mfalme Zumaridi kwa tuhuma za kuyageuza makazi yake kuwa kanisa na kuendesha shughuli za kidini bila usajili, kufanya mahubiri kwa waumini wake kwa sauti ya juu katika makazi ya watu na kusababisha usumbufu kwa majirani wanaoishi karibu na makazi yake.
Kwa mujibu wa taarifa ya iliyotolewa leo Mei 15,2025 na Jeshi hilo, Mfalme Zumaridi (42), amekamatwa saa nne asubuhi Mtaa wa Buguku, Buhongwa wilayani Nyamagana.
Taarifa hiyo imesema pia mwanamke huyo anahojiwa kuhusiana na taarifa inayoendelea kusambaa katika mitandao ya kijamii akionekana kwenye picha mjongeo akiwa na kundi la watoto wenye umri mdogo wa jinsia ya kike na kiume akiwaeleza kuwa yeye ndiye Mungu wao ambaye ana uwezo wa kuwatenganisha na kifo.
“Uchunguzi kuhusiana na tukio hili unaendelea, Jeshi la polisi katika uchunguzi huo litashirikiana na taasisi nyingine za serikali; hivyo linawaomba wananchi wenye taarifa mbalimbali zinazoweza kusaidia uchunguzi wa tuhuma hizi wafikishe kwa Jeshi la polisi. Uchunguzi utakapokamilika hatua za kisheria zinazostahili zitachukuliwa,” imesema.