21.4 C
New York

Jaji Kiongozi apongeza ushirikiano wa Mahakama na OSHA katika kukuza usalama na afya mahali pa kazi

Published:

Na Mwandishi Wetu, Gazetini

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Dk. Mustapher Siyani, amepongeza ushirikiano unaoendelea baina ya Mahakama na Wakala wa Usalama na Afya Mahali pa Kazi (OSHA), akisema ni muhimu katika kufanikisha utekelezaji wa majukumu ya Taasisi hizo mbili za serikali.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Dk. Mustapher Mohamed Siyani akizungumza na watumishi wa Mahakama Kuu Kanda ya Kati wakiwemo Majaji Wafawadhi, Majaji, Wasajili, Manaibu Wasajili, Mahakimu, Watendaji wa Mahakama na Wasaidizi wa Majaji wakati akifungua mafunzo kwa watumishi hao yaliyoandaliwa na OSHA kwakushirikiana na Mahakama Kuu-Divisheni ya Kazi na kuwezeshwa na OSHA.

Dk. Siyani alitoa pongezi hizo alipokuwa akifungua mafunzo maalum kwa Watendaji wa Mahakama Kanda ya Kati, yaliyobeba kauli mbiu: “Nafasi ya Teknolojia na Akili Bandia Mahali pa Kazi (Fursa na Mapinduzi)”, yaliyoandaliwa na OSHA kwa kushirikiana na Mahakama Kuu – Divisheni ya Kazi, na kufanyika katika Ukumbi wa OSHA jijini Dodoma kuanzia Aprili 23 hadi 24, 2025.

Mafunzo hayo yamehudhuriwa na zaidi ya washiriki 100 wakiwemo Majaji Wafawidhi, Majaji, Wasajili, Manaibu Wasajili, Mahakimu, Watendaji wa Mahakama, na Wasaidizi wa Majaji.

Katika hotuba yake, Jaji Kiongozi alisema:

“Niwashukuru OSHA kwa kuendelea kuwezesha mafunzo haya kwa watumishi wa Mahakama. Kwa kumbukumbu zangu, mwezi Desemba mwaka jana tulikutana hapa hapa kwa mafunzo kama haya. Mwendelezo huu ni jambo la kuigwa na Taasisi nyingine,” amesema Dk. Siyani.

Aidha, alisisitiza umuhimu wa mafunzo hayo, akibainisha kuwa mada zilizotolewa—ikiwemo Sheria ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi na matumizi ya teknolojia ya akili bandia—zina umuhimu mkubwa kwa watumishi wa Mahakama ambao ni wadau muhimu katika utoaji wa haki.

Aliongeza kuwa dunia inaelekea kwenye matumizi makubwa ya teknolojia, hivyo Tanzania haiwezi kujitenga na mwelekeo huo, hasa katika sekta ya Mahakama.

Akihitimisha hotuba yake, Dk. Siyani aliwashukuru washiriki kwa kujitolea muda wao kuhudhuria mafunzo, huku akitarajia kuwa maarifa waliyoyapata yataongeza ufanisi na tija katika utendaji kazi wao.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi, Dk. Yose Mlyambina akisisitiza jambo kwa watumishi wa Mahakama Kuu Kanda ya Kati wakiwemo Majaji Wafawadhi, Majaji, Wasajili, Manaibu Wasajili, Mahakimu, Watendaji wa Mahakama na Wasaidizi wa Majaji wakati wa ufunguzi wa mafunzo yaliyoandaliwa na OSHA kwakushirikiana na Mahakama Kuu-Divisheni ya Kazi na kuwezeshwa na OSHA jijini Dodoma.

Kwa upande wake, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu – Divisheni ya Kazi, Dk. Yose Mlyambina, alisema Mahakama Kuu inaendelea kujivunia uhusiano mzuri uliopo baina yao na OSHA, uhusiano ambao umekuwa ukizidi kuimarika na kuwavutia wadau mbalimbali wa sekta ya haki kazi.

Naye Mtendaji Mkuu wa OSHA, Khadija Mwenda, alisema mafunzo hayo yana faida maradufu kwa watumishi wa Mahakama kwani siyo tu yanawajengea uelewa wa masuala ya usalama na afya kama wafanyakazi, bali pia yanawasaidia katika kushughulikia kesi zinazohusu masuala hayo.

Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Usalama na Afya Mahali pa Kazi (OSHA), Khadija Mwenda akiwaeleza watumishi wa Mahakama Kuu Kanda ya Kati kuhusu wajibu na majukumu ya taassisi ya OSHA katika kulinda nguvu kazi nchini.

Mafunzo haya ni mwendelezo wa mafunzo yaliyotolewa awali Desemba 16-17, 2024, yaliyohusu Usalama, Afya, Haki na Wajibu kwa Watu Wenye Ulemavu.

Related articles

spot_img

Recent articles

spot_img