20.4 C
New York

Visual| Asilimia 26 ya watoto waliozaliwa miaka mitano kabla ya 2010 hawakutarajiwa

Published:

Na Mwandishi Wetu, Gazetini

Kwa mujibu wa Utatifi wa Demografia na Afya Tanzania wa mwaka 2010 ulikadiria kuwa asilimia 26 ya watoto waliozaliwa katika kipindi cha miaka mitano kabla ya utafiti huo hawakutarajiwa.

Hii ni sawa na kusema kwamba asilimia 26 ya watoto waliozaliwa mwaka 2005 nchini Tanzania hawakutarajiwa.

Utafiti huo unaenda mbali kwa kubainisha kuwa sababu za msingi za kiwango cha juu cha mimba zisizotarajiwa na za vijana ni pamoja na ufahamu mdogo wa upangaji wa uzazi na upatikanaji duni wa vifaa vya afya ya uzazi.

Sababu nyingine ni upatikanaji mdogo wa wahudumu wa afya wenye ujzui na uhaba wa raslimali zinazotolewa kwa ajili ya afya ya uzazi.

Hata hivyo, hali inaonyesha kuwa vituo vingi vya afya nchini bado vimekuwa na upungufu wa vifaa tiba kwa ajili ya kusaidia uzazi wa mpango.

Asilimia kubwa ya vituo vya afya vya umma nchini Tanznaia ambavyo vinakabiliwa na ukosefu wa vifaa vya uzazi wa mpango inaonyesha kutokidhi mahitaji ya upangaji uzazi.

Mapungufu makubwa yanabainika katika ufadhili wa kila mwaka wa uzazi wa mpango. Msichana ambaye anataka kupanga uzazi anaweza kwenda kwenye kituo cha afya cha eneo lake na kukuta kwamnba aina anazopendelea za uzazi wa mpango hazipatikani.

Wakati hali ikiwa hivyo, utafiti wa Afya ya Uzazi na Mtoto Viashiria vya Malaria Tanzania wa mwaka 2015-16 unaonyesha kuwa takribani wanawake 4 kati ya 10 sawa na asilimia 38 walioolewa na wenye miaka 15-49 kwa sasa wanatumia njia yoyote ya uzazi wa mpango, aidha, asilimia 32 wanatumia njia ya kisasa na asilimia 6 wanatumia njia ya asili.

Aidha, njia ya kisasa inayotumika zaidi kuliko zote ni ile ya sindano kwa asilimia 13 ikifuatiwa na vipandikizi kwa asilimia 7 na vidonge kwa asilimia 6.

Hatua hiyo ni bayana kwamba inakwamisha ndoto na malengo ya Tanzania ya kutaka kufanya vizuri zaidi kwa wanawake na wasichana.

Hata hivyo, katika kuhakikisha kuwa Tanzania inatimiza lengo hilo la kuwezesha jamii kuwa na uwezo wa kupanga ni wakati gani wapate mtoto mapema mwezi huu imepokea vifaa tiba vya uzazi wa mpango vyenye thamni ya dola milioni 4.5 kutoka kwa Shirika la Umoja wa Mataifa la Idadi ya Watu na Afya ya Uzazi(UNFPA) ambapo vitasambazwa katika vituo mbalimbali vya afya nchini Tanzania.

Akizungumza wakati wa Makabidhiano hayo ambayo yamefanyika Julai 18, 2022 Bohari Kuu ya Dawa(MSD) Keko Dar es Salaam, Mwakilishi Mkazi wa UNFPA, Mark Bryan Schreiner amesema vifaa hivyo vitasidia watu binafsi kuwa na uwezo wa kufanya maamuzi juu ya afya zao za uzazi, pindi na wakati sahihi wa kupata watoto.

“Vifaa hivi vinatoa njia za uwezeshaji binafsi, hasa kwa wanawake na wasichana. Lengo letu la pamoja ni usambazaji wa dawa hizi za uzazi wa mpango na vifaa vya afya ya uzazi kwa maelfu ya vituo vya afya, hospitali, zahanati na huduma za kijamii, kisha kusambazwa ili kutoa haki na chaguo za upangaji uzazi kwa wanawake na wanaume kote nchini.

“Tunaipongeza Serikali ya Tanzania kwa dhamira ya FP2030 ya kuendeleza uzazi wa mpango unaozingatia haki na ongezeko lililopangwa la 10% la kila mwaka katika mgao wa sasa wa Sh bilioni 14 za Tanzania zitakazotolewa kikamilifu kwa ajili ya ununuzi wa vidhibiti mimba,” amesema Mark na kuongeza kuwa:

“Kupitia ushirikiano wa UNFPA wa Ugavi, tunatazamia kushirikiana zaidi na Tanzania mwaka huu ili kuanzisha maelewano ya nchi na kuimarisha dhamira yetu ya pamoja ya ufadhili wa siku zijazo kwa ajili ya vifaa vya afya ya uzazi. Hii ni hatua muhimu na endelevu wa uzazi wa mpango nchini Tanzania,” amesema Mark.

Related articles

spot_img

Recent articles

spot_img