22.9 C
New York

Infographic| Makundi Afcon 2021, ni vita ya kibabe!

Published:

AGOSTI 17, 2021, ilichezeshwa droo ya hatua ya makundi ya fainali za Afcon 2021 zinazotarajiwa kuanza kutimua vumbi Januari 9, mwakani. Jina ‘Afcon 2021’ limetokana na ukweli kwamba michuano hii ilitarajiwa kuchezwa mwaka huu lakini ikapigwa kalenda kutokana na janga la Corona.

Ukiacha zile za mwaka 2019, hii ya mwakani itakuwa mara ya pili kwa fainali hizo kushirikisha timu 24, tofauti na zile 16 zilizokuwa zikipata nafasi hapo awali.

Michuano hii itafanyika Cameroon, miji mitano ikiwa mwenyeji, ambapo mechi zitachezwa katika viwanja sita. Miji itakayokuwa ‘bize’ kwa kipindi cha mwezi mmoja wa mashindano ni Yaounde, Limbe, Daoula, Bafoussam, na Garoua.

Kufuzu ilikuwaje?

Katika kusaka timu 24, zilikuwapo 52 zilizocheza mechi za kuwania tiketi ya kucheza fainali hizi za Afcon 2021. Michezo ya kufuzu ilianza Oktoba, 2019, na kumalizika Juni, 2021.

Huku fainali za mwakani zikiwa za 33 tangu zilipoanzishwa na Shirikisho la Soka Afrika (CAF), kuna timu mbili (Comoros na Gambia) zitakazokuwa zinashiriki kwa mara ya kwanza.

Malawi wamerejea baada ya kutoshiriki kwa miaka 11. Ethiopia, mabingwa wa mwaka1962, hawajalibeba taji hili la Afcon tangu mwaka 1976. Guinea-Bissau wameshiriki Afcon kwa mara ya tatu mfululizo lakini hawajawahi kushinda hata mechi moja kwenye michuano hiyo.

Makundi yakoje?

Safari hii, katika droo iliyofanyika Cameroon ambako ndiko zitakakofanyika fainali hizi, timu 24 zilizokata tiketi ziligawiwa kwenye makundi sita.

Kundi A: Cameroon, Burkina Faso, Ethiopia, Cape Verde

Kundi B: Senegal, Zimbabwe, Guinea, Malawi

Kundi C: Morocco, Ghana, Comoro, Gabon

Kundi D: Nigeria, Egypt, Sudan, Guinea-Bissau

Kundi E: Algeria, Sierra-Leone, Guinea ya Ikweta, Ivory Coast

Kundi F: Tunisia, Mali, Mauritania, Gambia

Nani kusonga 16 bora?

Kama ilivyo kawaida, baada ya kila timu kucheza mechi tatu za hatua ya makundi, mbili zitakazomaliza katika nafasi za juu zitaingia moja kwa moja 16 bora.

Kwa hesabu za kawaida, hapo zitapatikana timu 12, ambapo nne za kukamilisha zile 16 ni zile zilizofanya vizuri lakini zikaishia nafasi ya tatu (best losers).

Hata hivyo, inafahamika kuwa kila msimu huwa kuna timu zinazotazamwa zaidi. Je, ni Cameroon, Senegal, Morocco, Ghana, Nigeria, Misri, Algeria, Ivory Coast, Tunisia au Mali?

Itoshe kusema katika timu hizo shiriki, 14 zinaingia kwenye mashindano haya zikiwa zimeshawahi kutwaa ubingwa.

Rekodi zinazofukuziwa

Kwa ufupi, unaweza kujiuliza; nani atavunja rekodi ya Samuel Eto’o, mfungaji bora wa muda wote wa Afcon? Akiwa na Cameroon kabla ya kustaafu, alifunga jumla ya mabao 18 kwa misimu yake sita kwenye michuano hiyo.

Hadi sasa, anayeweza kuvunja rekodi hiyo kwa kuwa bado anacheza soka ni Andre Ayew (Ghana) mwenye mabao tisa. Kwamba afunge zaidi ya mabao tisa Afcon 2021!

Pia, nani atakayevunja rekodi ya mkongwe wa Misri, Ahmed Hassan? Huyo ndiye mchezaji pekee kuwahi kuibeba mara mbili mfululizo tuzo ya mchezaji bora wa mashindano ya Afcon akifanya hivyo mwaka 2006-2010.

Katika michuano iliyopita, ni kipa wa Algeria, Rais M’Bolhi, ndiye aliyeibeba. Je, atainyakua tena na kuvunja rekodi iliyodumu kwa muda mrefu?

Algeria kutetea ubingwa?

Ni swali gumu kwa sasa lakini Algeria ya kocha mzawa, Baghdad Bounedjah, itaingia kwenye michuano hii ikitaka kulibeba kwa mara ya pili mfululizo taji hilo.

Algeria ilitwaa ubingwa wa mashindano yaliyopita, mwaka 2019, kwa kuifunga Senegal bao 1-0 katika mtanange wa fainali. Hadi sasa, Algeria hawajafungwa katika mechi 27.

Endapo vigogo hao wa soka la Kaskazini mwa Bara la Afrika watafanikiwa kulitetea Kombe hilo, basi watafuata nyayo za Waarabu wenzao, Misri, waliofanya hivyo mwaka 2010.

Related articles

spot_img

Recent articles

spot_img