21.8 C
New York

Visual| Idadi ya Watoto Tanzania kabla ya Sensa 2022

Published:

Na Faraja Masinde, Gazetini

Agosti 23, mwaka huu Tanzania inatarajia kufanya Sensa ya Watu na Makazi ikiwa ni sensa ya sita kufanyika tangu Muungano wa Tanganyika na Zanzibar.

Umuhimu wa zoezi hilo nikwamba takwimu zitakazopatikana zitatumiwa na Serikali katika utungaji, ufuatiliaji na uboreshaji wa sera mbalimbali pamoja na kufanya maamuzi kwa kuzingatia vigezo vya kitakwimu.

Kwa kutambua idadi ya watu na shughuli wanazofanya inasaidia serikali kujipanga vyema katika ugawaji wa rasilimali.

Takwimu rasmi zitaiwezesha serikali kukabiliana na changamoto mbalimbali zitakazojitokeza katika sekta zote za kiuchumi, kwa kuwa zitatoa viashiria vya uwajibikaji ndani ya serikali.

Hata hivyo, wakati tukielekea kwenye zoezi hilo, fahamu kuwa Ofisi ya Taifa ya Takwimu(NBS) mwaka 2021 ilitoa makadirio ya idadi ya watu nchini.

Kwa mujibu wa ripoti ya hali ya uchumi wa Taifa Mwaka 2020, iliyotolewa na NBS mwaka 2021, idadi ya watu Tanzania iliongezeka kwa asilimia 3.1 na kufikia watu 57,637,628 ikilinganishwa na watu 55,890,747 mwaka 2019.

Ripoti hiyo ilieleza kuwa kwa mwaka 2020 Tanzania Bara ilikadiriwa kuwa na watu 55,966,030, sawa na asilimia 97.1 ya watu wote na Tanzania Zanzibar ilikadiriwa kuwa na watu 1,671,598 sawa na asilimia 2.9.

Kati ya idadi hiyo watoto wenye umri kuanzia miaka 0 hadi 19 walikadiriwa kuwa 31,040,164 sawa na asilimia 53.85 ya watu wote nchini Tanzania.

Kwa mujibu wa makadirio hayo ya NBS ni wazi kuwa idadi kubwa ya watu nchini ni watoto kuanzia umri 0 hadi miaka 19 kwani inachukua asilimia 53.85 ya watu wote. Aidha idadi ya wakuanzia miaka 20 na kuendelea ni  26,597,464 sawa na asilimia 46.15 tu.

Hivyo, pamoja na changamoto za utafutaji wa maisha ya kila siku zoezi la kuhesabiwa ni muhimu kwa manufaa yako na taifa kwa ujumla kwani linarahisisha serikali kusukuma maendeleo kutokana na kujua idadi ya watu.

Zaidi fuatilia usanifu wetu ambao umechambua idadi ya watoto kwa umri nchini Tanzania kabla ya Sensa inayotarajiwa kufanyika Agosti 23, nchini kote..

Related articles

spot_img

Recent articles

spot_img