Na Mwandishi Wetu
Rais Samia Suluhu Hassan ameongoza Harambee ya kuchangia ujenzi wa Kituo cha Watoto wenye mahitaji Maalum cha Bagamoyo Diaconic Lutheran Centre ambapo amechangia Sh 150 milioni, kwa ajili ya ujenzi wa kituo hicho cha Watoto wenye mahitaji maalumu kinachotarajiwa kujengwa na Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania(KKKT) Dayosisi ya Mashariki na Pwani mkoani Pwani.
Pia washauri wa Rais wamechangia Sh 100 milioni, hivyo kufanya ofisi ya Rais kuchangia Sh 250 kwa ajili ya ujenzi wa kituo hicho.

Akizungumza katika Harambee hiyo Rais Samia amemhakikishia Mkuu wa Kanisa hilo, Askofu Dk Alex Malasusa kuwa serikali itaendelea kushirikiana bega kwa bega katika hatua zote za ujenzi pamoja na uendeshaji wa kituo hicho.
“Kiwango nilichojiwekea kuchangia katika shughuli za kanisa ni Sh milioni 100, lakini nikivaa kofia ya bibi nitachangia Sh milioni 50, na wasaidizi wangu wamejichanga na kuchangia Sh milioni 250, hivyo kama ofisi yangu tunachangia Sh milioni 250,”

Aidha Rais Samia amesisitiza kuwa matendo chanya yanayofanywa na baadhi ya watumishi wa dini yanaonyesha mfano bora kwa wengine wanaojiita watumishi wa dini, lakini hawaleti manufaa kwa jamii.
Pia amehimiza ushirikiano wa wazazi wote wawili katika malezi ya watoto wenye changamoto, akisema ni jukumu la familia nzima.
“Nasimama mbele yenu kama mama ambaye nabeba dhamana ya malezi kama mama, si tu wa mahaitaji maalumu bali wote, ninasimama nikiwa naelewa fika jukumu kubwa wanalolibeba akina mama wanapokuwa na watoto wenye uhitaji maalumu,” amesema Rais Samia.
Ameeleza dhamira ya Serial kuendelea kushirikiana na wadau wa maendeleo wakiwamo viongozi wa dini na mashirika yasiyo ya kiserikali, kuhakikisha upatikanaji wa huduma bora kwa watoto wenye mahitaji

Kwa upande wake Mkuu wa KKKT, Askofu Dk Alex Gehaz Malasusa amemshukuru Rais Samia kwa mchango wake na uwepo wake katika harambee hiyo akisema unaleta ujumbe kwamba walemavu ni sehemu ya taifa na wanahaki ya elimu na kujifunza.
Amesema tayari kanisa hilo limeanza michoro ya usanifu wa majengo na imekamilika, huku ikikusanya Sh 2.7 bilioni kupitia harambee ya ndani iliyojumuisha sharika na mitaa mbalimbali.