17.6 C
New York

Rais Samia aongoza  mazishi ya Hayati Cleopa Msuya,  ataja mambo ya kujifunza

Published:

Na Mwandishi Wetu, Gazetini

Rais Samia Suluhu Hassan ameongoza mazishi ya aliyekuwa Makamu wa Kwanza wa Rais na Waziri Mkuu wa Tanzania, Hayati Cleopa Msuya na kusisitiza kuendelea kuenzi na kujifunza kwa yale aliyoyafanya kipindi cha uhai wake.

Ameyasema hayo leo Mei 13,2025 katika ibada ya mazishi ya Hayati Msuya iliyofanyika katika  Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Kristo Mchungaji Mwema, Usharika wa Usangi Kivindu, Mwanga,  mkoani Kilimanjaro.

Rais Samia ameyataja baadhi ya mambo ambayo kama viongozi wanapaswa kujifunza kuwa ni kupenda maendeleo na  kuwa na msimamo bila kuyumbishwa na chochote,kufanya kazi kwa uzalendo, uadilifu na uaminifu.

Ametaja mambo mengine kuwa Hayati aliamini kwamba ujuzi na utaalamu una nafasi kubwa katika kuleta maendeleo, pia hakuwa muoga wa mabadiliko, aliamini mabadiliko ni hatua katika maendeleo na alikuwa na uvumilivu.

Aidha katika kumuenzi, Rais Samia ameahidi kuchangia  ujenzi wa kituo cha afya kilichopo Wilaya ya Mwanga ambacho Hayati Msuya alianzisha  ujenzi wake.

“Katika kuangalia aliyoyafanya Mzee Msuya kuna kijiji hapa alianzisha ujenzi wa kituo cha afya na akawataka Wanamwanga wote kwa pamoja kukusanya nguvu kujenga kile kituo, wito wangu kwenu tumalizeni kile kituo, wote tuchangie na mimi nitachangia. Tumalize na kile kituo na tukipe jina lake, hiyo ndiyo kumuenzi Mzee wetu,” ameeleza Rais Samia.

Naye Rais Mstaafu wa Dk, Jakaya Kikwete amemuelezea Hayati Msuya kuwa kiongozi  aliyekuwa makini na  mvumilivu kutokana na mambo mbalimbali magumu aliyopitia katika kipindi cha uongozi wake.

“Mzee Msuya ni mtu aliyejaaliwa akili kubwa lakini alifahamu mambo ya fedha na uchumi sana kama vile ni mchumi mbobezi hili ndiyo la kujifuza. Alikuwa Waziri  wa fedha katika kipindi kigumu cha uchumi. Kulikuwa na uhaba mkubwa wa fedha za kigeni kwa sababu uchumi ulikuwa umedumaa na chamaoto kubwa za upatikanaji wa huduma za kijamii.

“Mzee Msuya kama Waziri wa fedha alikuwa na juhudi kubwa ya kuzuia mambo yasiharibike zaidi, alifanyaje alikuwa anayajua yeye zaidi.
Alikuwa mwenye akili na maarifa mengi,” Ameelezea Dk. Kikwete.

Kwa upande wake, Makamu wa Rais Dk. Phillip Mpango, amesema mara ya mwisho alipokutana naye  alimkumbusha awaambie viongozi wenzake wajitahidi kufuata wananchi kule walipo ili kutatua kero zao.


Related articles

spot_img

Recent articles

spot_img